Friday 27 May 2016

‘Wafugaji wasipodhibitiwa watachunga hadi Ikulu’


Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Kessy.   MBUNGE wa Nkasi Kaskazini, Ally Mohamed Keissy (CCM) amesema kama wafugaji wataachwa waendelee kuzurura ovyo nchini, ipo siku watachunga ng’ombe hadi Ikulu. Aidha, wabunge jana na juzi wameungana na kueleza kuwa siyo sahihi kwao kuendelea kunyoosheana vidole kati yao kuhusu migongano ya wakulima na wafugaji badala yake serikali ije na mkakati wa kupanga matumizi bora ya ardhi, kwani wote wanahitajika.
Akichangia hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii juzi bungeni, Keissy alisema si sahihi kuwaacha wafugaji waendelee kuchunga kila eneo nchini bila kuwa na udhibiti maalumu. “Tunasema asilimia 75 ya Watanzania ni wakulima, kwa hiyo kama wengi ni wakulima, sasa kama ni kumjali basi tumjali mkulima kwani mvua zikikosekana kwa kuharibu mazingira, hatuna uwezo wa kilimo cha umwagiliaji”.
Hatuwezi kuendelea kutishana humu ndani. Lazima wafugaji wafuge kwa kufuata taratibu. Tukiwaachia hawa ipo siku wafugaji watachunga ng’ombe hadi Ikulu,” alisema Keissy.
Akizungumzia ujangili, mbunge huyo matata alisema ni vyema askari wanyamapori akikuta mtu ameingia katika hifadhi bila ruhusa, ampige risasi kwa sababu akimwacha anauawa yeye (askari).
Kwa upande wake, Mbunge wa Muhambwe, Atashata Nditiye (CCM), alisema lazima wabunge waache siasa na kuweka mbele maslahi ya Taifa vinginevyo nchi itageuka jangwa.
Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa (Chadema) alisema badala ya kugombana, lazima maslahi ya Taifa yawekwe mbele na kuwapo na mipango madhubuti ya kutenga maeneo ya wakulima, wafugaji, samaki na shughuli nyingine za kiuchumi.

No comments:

Post a Comment