Thursday 2 February 2017

Wanawake ni nguzo ya jamii na uchumi wa nchi, asema Ruto

Naibu Rais William Ruto katika kongamano. Ruto anataka wanawake kupewa nafasi sawa katika jamii ili kuiendeleza. [Nation/www.nation.co.ke] Naibu Rais William Ruto amebaini kuwa Afrika haiwezi kuendelea kwa kumdhalilisha mwanamke, ila tu kwa kumpa nafasi murwa ya kujiendeleza katika sekta zote za maisha.
Ruto, katika ukurasa wake wa Facebook amefafanua kuwa dunia inadororesha sekta mbali mbali kwa kutomhusisha mwanamke katika maswala ya kiuchumi. "Kongamano hili litumike katika kuimarisha nafasi ya mwanamke katika masuala ya uchumi na biashara kote duniani ili kujiendeleza kimaisha," alisema Ruto. Naibu wa rais amesisitiza kuwa wanawake humu nchini wanendelea vizuri katika maswala ya kiuchumi hasa kutokana na kuwawezesha kupata huduma za mikopo pamoja na mpango wa fedha za Uwezo. “Huduma kwa wanawake, watu wenye ulemavu pamoja na vijana wameendelea kibiashara, swala ambalo lina umuhimu sana kwa maendeleo ya taifa hili,” aliongeza Ruto. Ujumbe wake vile vile umeungwa mkono na Rais wa Liberia Ellen Johnson Sirleaf, ambaye ametaja kuwa uhuru wa kumiliki ardhi kwa wanawake ni jambo ambalo linapaswa kushughulikiwa kiundani sana maanake ardhi ndio nguzo muhimu katika uzalishaji. Sirleaf ameongeza kuwa mwanamke ni nguzo ya jamii, huku akitoa mfano wa taifa lake la Liberria ambamo kupitia kwa mshikamano wa wanawake, taifa hilo limepata nafuu kutokana na hali ya utovu wa amani ambayo ilikuwa imelikumba kwa takriban miaka miwili.