Wednesday 2 March 2016

Wanawake wanaweza wakiandaliwa mazingira-TGNP


 Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Loyola ya jijini Dar es Salaam wakifuatilia mada mbalimbali ndani ya maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shule ya Sekondari Loyola.
 Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Bi. Lilian Liundi akizungumza na wanahabari kwenye maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shule ya Sekondari Loyola.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Loyola wakionesha ubunifu wa mavazi katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shuleni hapo.

 Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Bi. Lilian Liundi akizungumza na wanahabari kwenye maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shule ya Sekondari Loyola.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Loyola wakionesha ubunifu wa mavazi katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shuleni hapo.
 Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Bi. Lilian Liundi akizungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Wanawake Shule ya Sekondari Loyola ya jijini Dar es Salaam leo.






KAIMU Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Bi. Lilian Liundi amesema wanawake wanaweza kuwa viongozi wazuri na mfano wa kuigwa katika maeneo mbalimbali endapo watajengewa mazingira na kuandaliwa mapema tangu wawapo shuleni.



Bi. Liundi ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya TGNP ametoa changamoto hiyo leo katika Shule ya Sekondari ya Loyola ya jijini Dar es Salaam alipokuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya mwanamke shuleni hapo.



Akizungumza na umati wa wanafunzi wasichana wa shule hiyo na wageni anuai waalikwa, alisema tafiti nyingi zilizofanywa zinaonesha kuwa wasichana wanapoandaliwa mazingira mazuri ya elimu wanafanya vizuri ukilinganisha na wavulana.



Aidha aliongeza kuwa kwa sasa zipo shule zinazochukua wasichana pekee ambazo zimekuwa zikifanya vizuri zaidi jambo ambalo linaonesha wazi mazingira mazuri yakijengwa jamii hii inaweza kuinuka na kuwa mfano mzuri.



Alisema kwa sasa vishawishi na changamoto anuai zilizopo katika shule nyingi ndio kikwazo kwa wanafunzi wa kike kufanya vizuri, hali ambayo ikifanyiwa kazi kiufasaha mabadiliko kimafanikio kwa kundi hilo yanaweza kutokea.



Hata hivyo alisema tafsiri iliyojengeka ya kwamba wanafunzi wa kike wanaogopa masomo ya sayansi si sahihi kiuhalisia, kwani mazingira ambayo wanafunzi hawa wanakumbana nayo ndio kikwanzo katika mafanikio yao kimasomo.



“Mfano shule nyingi za kata ni za kutwa wanafunzi hasa wasichana wanakaa mbali na shule, wanalazimika kutembea umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni…wanakumbana na changamoto nyingi njiani hivyo wanajikuta wanashindwa kufanya vizuri au kukatishwa kabisa masomo yao,” alisema Bi. Liundi.



Aliongeza kuwa eneo kama hili, vyombo husika vikiangalia sheria na sera zinazojenga mazingira mazuri kwa makundi yote, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha rasilimali zilizopo zinatumika vizuri wasichana wanaweza kuingia katika ushindani kwa fursa zilizopo.



Kwa upande wake mwanafunzi Grace Ntambi wa kidato cha tano wa shule hiyo aliiomba serikali kuendelea kutoa elimu kwa mikoa ambayo bado inaendeleza mila potofu za kumbagua mtoto wa kike ikiwa ni pamoja na kuelemea kwenye mfumo dume, ili kuangamiza vitendo hivyo.



“Na hii ianzie pia katika ngazi za familia kuna kila sababu ya kuondokana na mila potofu za kwamba mtoto wa kike hana haki ya kupata elimu kama ilivyo kwa mtoto wa kiume…tuwatie moyo wasichana kwani wanaweza,” alisema mwanafunzi huyo.



Katika hafla hiyo pia TGNP ilipata fursa ya kutoa mada mbalimbali za masuala ya wanafunzi kujitambua kwa hatua anuai ikiwa ni pamoja na kutoa ushuhuda ya kwamba wanawake wanaweza wakiamua kufanya hivyo kwa kila hatua wanayopiga.

No comments:

Post a Comment