Wednesday 8 June 2016

NAMNA INAYOFAA YA KUSHUGHULIKA NA MALALAMIKO

WATU wengi wamejaribu kuwashawishi wengine jinsi wanavyofikiri kufanya kwa kuzungumzia zaidi kuhusu mambo yao. Waache na wengine wazungumze.

Kwani wanajua zaidi kuhusu shughuli zao na matatizo kuliko unavyodhani. Kwa hiyo ni vema uendelee kuwauliza maswali ili waweze kukwambia mambo machache wanayoyajua.
Watu wengi hujikuta wakiingilia kati pale ambapo hawakubaliani na mazungumzo ya mwingine. Lakini wewe usifanye hivyo. Ni hatari. Hawatakusikiliza wakati bado wana mawazo yao mengi ya kueleza.
Hivyo ni vema kusikiliza kwa utulivu na kuweka kumbukumbu kile kinachozungumzwa. Kuwa mtulivu katika hilo. Watie moyo kuelezea mawazo yao yote.
Je, unafikiri utaratibu huo ni mzuri? Hebu tumuangalie mfanyabiashara. Kulikuwa na mfanyabiashara moja ambaye alikuwa akitafuta soko kwa ajili ya biashara yake, kabla ya kumwona mhusika mkuu wa ofisi aliyokuwa anakwenda, alipata tatizo la kukaukiwa na sauti yake.
Alipopata nafasi ya kuonana na Mkurugenzi huyo wa kampuni aliyokwenda, aliandika kwenye karatasi kumweleza kuwa sauti yake imekauka na kumuuliza kama wanaweza kuendelea katika hali hiyo aliyonayo na mhusika yule akamwambia kwamba wanaweza kuendelea na mazungumzo yao.
Hivyo, alitoa nyaraka mbalimbali za uthibitisho wa bidhaa zake, ambapo Mkurugenzi yule alipokuwa akizipitia alikuwa akitabasamu kwa kuonyesha kuwa anakubaliana na bidhaa hizo.
Alimpongeza mfanyabiashara huyo kwa kuwa na bidhaa nzuri na kuamua kusaini naye mkataba. Baada ya kutiliana saini, mfanyabiashara alisema tangu aanze biashara yake hiyo hajawahi kupata kazi yenye mkataba wa fedha nyingi kama ulivyo huo.
“Ninajua kuwa ningepoteza mkataba huu kama sauti yangu isingekauka, kwa sababu nilikuwa na mawazo tofauti katika mazungumzo yote tuliyoyafanya.
“Nimegundua kuwa kukauka sauti kwangu kwa bahati mbaya, kumenipatia utajiri mkubwa, hivyo wakati mwingine ni vyema kuwaacha watu wengine wazungumze,” anasema mfanyabiashara huyo.
Kuwaacha watu wengine wazungumze kunasaidia katika mazingira ya familia pia kwenye biashara. Mfano mwingine ni wa mama mmoja na mtoto wake Lilly ambao walikuwa hawana mahusiano mazuri.
Lily alikuwa ni mtoto mkimya asiyependa kuzungumza, lakini alikuwa hana uhusiano mzuri na mama yake wakati wa ukuaji wake, kwa kuwa mama yake alikuwa akimtishia na kumwadhibu pasipo sababu za msingi.
Kutokana na adhabu hizo mtoto huyo alikuwa akimwangalia tu mama yake, na mama huyo alipokuwa akimgombeza mtoto huyo alimwangalia tu na kuondoka eneo hilo.
Siku moja mama huyo aliwaambia wenzake kuwa mtoto wake amemshinda hivyo amenawa mikono juu yake. ” Mtoto huyu amenishinda amekuwa akiondoka nyumbani na kwenda kwa rafiki yake wa kike bila kuaga, lakini aliporudi nilikosa nguvu ya kumwadhibu tena, nilimwangalia kwa huzuni na kumuuliza kwa nini Lilly unafanya hivi?,” anasema mama huyo.
Kwa maelezo ya mama huyo, mtoto wake alimwangalia kwa upole na kumuuliza, “Je ni kweli unataka kujua?,” mama huyo anasema kwanza alimwangalia mtoto wake na kuanza kupatwa na wasiwasi, baada ya muda wasiwasi huo ukatoweka. Hakuwa tayari kumsikiliza, japo amekuwa mara nyingi akimwambia mtoto huyo kufanya kile na kile.
Mama huyo anasema wakati mtoto Lilly alipokuwa anamweleza mawazo na hisia zake, aliingilia kati na kutoa mamlaka nyingi kumzuia asiendelee kuzungumza.
Lakini mama anasema aliaza kutambua kuwa mtoto huyo alimhitaji, si kwamba awe kama mama ambaye anajiona ni bosi, lakini mwenye ujasiri na hayo ndiyo matokeo ya kumchanganya katika makuzi yake. Na mtoto huyo alipokuwa akijaribu kuzungumza na mama yake, mama huyo hakuwa tayari kumsikiliza.
Baada ya kukaa na kutathmini mama huyo alijiona kuwa ana makosa katika malezi ya mtoto wake, kwani mtoto huyo alihitaji kusikilizwa na kuheshimiwa mawazo yake. Tokea siku hiyo mama huyo alimwacha mtoto wake kumweleza hisia zake na aliweza kumsikiliza.
“Tangu wakati huo na kuendelea nimekuwa nikimwacha mtoto wangu azungumze kile anachotaka. Ananishirikisha mambo yake na uhusiano wetu umeanza kuwa mzuri, amerudi kuwa mtu wenye ushirikiano,” anasema mama huyo.
Hivyo, ni jambo zuri kwa wazazi kuwa karibu na watoto wao, kujua nini wanapenda, upungufu wao na jinsi gani anaweza kumrekebisha kwa hekima pasipo kutumia jazba wala kujionyesha kuwa yeye ni bosi hivyo mtoto anapaswa kumsikiliza kwa kila jambo.
Malezi bora ni pale wazazi na watoto wanapoelezana jambo kwa uwazi, hekima na kusikilizana hata kufikia mwisho wa jambo lenyewe. Ni vema kutoa nafasi kwa wengine nao waweze kutoa mawazo yao.

No comments:

Post a Comment