Wednesday 1 June 2016

Ijue sheria ya uchumba: Ukivunjwa, Zawadi, Kushitaki, Umri na Muda

WATU wengi ambao huingia kwenye uhusiano wa kimapenzi, kwa kawaida uhusiano wao wa manzo huwa unatawaliwa na uongo mwingi pamoja na ahadi hewa.
Mara nyingi, ahadi hizo huwa ni nyingi mno, lakini kwa kadri ya makala haya, tutazungumzia ahadi moja tu, ya kuoana.


Katika hali ambayo ni ya kweli kabisa, kati ya watu 10 wanaoahidiana kuoana, ni watu wawili au mmoja tu ambao hutimiza ahadi hiyo.

Hii inatokana na sababu nyingi, lakini kubwa, ni watu kutokuwa wakweli tangu mwanzo wa uhusiano wao. Kwa hiyo, wengi wao huja kujitambua baadaye kwamba walikuwa wakidanganywa na wenza wao, na baya zaidi, ukweli huo wa kudanganyana unakuja kujulikana mwishoni kabisa wakati ambapo mtu huwa ametumiwa vya kutosha!

Pamoja na udanganyifu huo ambao ni mbaya sana ukitokea, watendewa huwa wanakaa kimya huku wakijilaumu wenyewe na hivyo kutoa laana nyingi kwa watu waliowatendea, jambo ambalo kimsingi halisaidii lolote.

Kwanini hali hiyo hutokea? Wengi wao huingia kwenye uhusiano bila kujua haki za kisheria zinazotawala katika uhusiano wao huo wa kimapenzi.

Sheria inaruhusu kushitaki uchumba unapovunjwa


Kuvunja ahadi ya kuoa au kuolewa, kwa maana ya kuvunja uchumba, ni kosa kisheria ambalo linaadhibiwa kwa fidia. Sheria haikukaa kimya na kuacha watu wachezewe halafu mambo yaishie hapo kama wafanyavyo wengi.

Sehemu ya tano, kifungu cha 69(1) cha Sheria ya Ndoa, inasema: “Shauri la fidiai linaweza kufunguliwa kwa mtu yeyote aliyevunja au kukiuka ahadi ya ndoa na haijalishi ahadi hiyo ilifanyika Tanzania au pengine.”

Jambo hili limewekwa katika sheria ili kulinda utu wa watu na kuthamini thamani ya mtu anayejitoa kumsubiri au kumngoja mwenzake kwa kutumaini jambo la kheri, kwa mfano ndoa.

Sheria inatambua kwamba katika kipindi hiki cha uchumba, watu hupoteza muda, hali pamoja na mali vitu ambavyo haviwezi kuachwa hivi hivi bila kulipiwa baada ya ahadi kuvunjwa.

Mchumba wa umri chini ya miaka 18 hachukuliwi hatua


Pamoja na hayo, kifungu cha 69(a), kimeweka sharti kwamba hakuna mtu yeyote atakayeweza kumchukulia hatua mtu ambaye wakati wanawekeana ahadi ya kuoana, alikuwa chini ya umri wa miaka 18.

Hii inatoa fundisho kwamba anayestahili kuchukuliwa hatua kwa kosa hilo la kuvunja uchumba, lazima awe ni yule ambaye wakati anaweka ahadi hiyo alikuwa amefikisha umri wa miaka 18. Kwa mujibu wa kufungu hicho, kama mmoja wa wenye uhusiano aliweka ahadi ya aina hiyo kabla ya kufikisha umri wa miaka 18, basi hakuna hatua dhidi yake zinazoweza kuchukuliwa kisheria.

Sheria inaruhusu zawadi zote za uchumba zirejeshwe


Kifungu cha 71 cha Sheria ya Ndoa kinafafanua kwamba: “Mtu anaweza kufungua shauri la kurejeshwa kwa zawadi ambazo wachumba walipeana bila mkataba, lakini baada ya Mahakama kuridhika kuwa mtoaji alitoa zawadi kwa nia na lengo la mkataba wa ndoa ambayo ingefungwa baadaye.”

Kwa kifungu hicho cha sharia, tunapata mambo mengi. Kwanza; ni pale kifungu hiki kinaposema kwamba zawadi ambazo wamepeana bila kuingia mkataba.

Neno ‘bila mkataba’ limewekwa kwa makusudi kwa kujua kuwa wengi ambao wangetakiwa kurejesha zawadi, na hasa zawadi tamu kama vile magari, nyumba, viwanja na kadhalika, wangeleta kinga kuwa mtu fulani aonyeshe ni wapi tuliwekeana makubaliano au mkataba!

Sasa kwa kulikwepa hilo ili watu wasikose haki zao kiholela, sheria ikaweka kuwa hata kama zawadi hizo zilitolewa bila kuingia mkataba wowote, lazima zitarejeshwa ili-mradi mtu adhibitishe kuwa alikuwa anazitoa kwa sharti la ndoa ambayo ingefungwa baadaye.

Suala la kwamba mchumba alitoa zawadi kwa sharti la ndoa, linaweza kuthibitishwa kwa njia mbalimbali kwa mfano barua, ujumbe mfupi katika simu pamoja na mashahidi mbalimbali.

Ni uchumba wa aina gani mtu anaruhusiwa kushitaki?


Ni muhimu kutambua kwamba uchumba unaostahili haki zote zilizotajwa hapo juu, si ule wa mazoea wa; utanioa? Ndiyo nitakuoa!

Uchumba wenye haki zote ni aina ya uchumba ambao upo katika kiwango cha kuitwa uchumba. Ni uchumba ambao uko makini (serious) na wa dhati kimazingira. Kwa maneno mengine, si kila mtu anayeitwa mchumba, basi anastahili haki hizo za fidia.

Mtu atatakiwa kuithibitishia Mahakama kiwango cha uchumba kabla ya kupewa haki yoyote. Yapo mambo ambayo yanaweza kuthibitisha uchumba wa kweli. Moja wapo ni kutambulishana kwa wazazi, ndugu na kadhalika.

Wengine walio makini kama wenzetu Wazungu, huwa wanaandikishana kabisa na hivyo inapotokea mmoja wao akavunja uchumba, maandishi hayo ynabakia kuwa ushahidi tosha na usio na utata.

Je; Mahakama inaweza kuamuru wachumba kurudiana?


Kutokana na kifungu cha 69(3) cha Sheria ya Ndoa, hakuna mchumba atakayeruhusiwa kupeleka shauri la kudai kutimizwa kwa ahadi hiyo ya kuoana. Kwa maneno mengine, mtu hawezi kwenda mahakamani kudai kwamba “Mimi siombi kitu kingine chochote Mheshimiwa Hakimu, bali naomba fulani anirudie na anioe tu, kama tulivyokuwa tumeahidiana mwanzoni.”

Kwa kawaida, ombi kama hilo huwa linatolewa katika mikataba mingine, lakini si katika masuala yanayohusiana na uchumba.

Mtu akishamfikisha aliyekuwa mchumba wake mahakamani asitarajie hata kidogo kuilazimisha Mahakama ili uchumba wao urudi ili waoane. Si kazi ya Mahakama kutoa hukumu ya kwamba fulani lazima amuoe fulani au lazima watu fulani warejeane.

Muda unaoruhusiwa kufungua shauri la madai


Jambo la mwisho katika uhusiano huo wa uchumba, linatokana na kifungu cha 70 cha Sheria ya Ndoa, ambacho kinatoa muda wa kufungua shauri la kuvunja uchumba.

Kwa mujibu wa kifungu hicho, shauri lolote linalohusiana na kuvunja uchumba, linapaswa kufunguliwa kwa muda ambao hauzidi mwaka mmoja tangu uchumba ulipovunjwa.

Mtu yeyote anayepeleka shauri kama hili baada ya mwaka mmoja tangu uchumba uvunjwe, anakuwa nje ya muda, na shauri hilo haliwezi kusimama.

1 comment: